Wakati raia tisa wa China wakibainika kuugua ugonjwa wa dengue na
kulazwa hapa nchini, Rais Jakaya Kikwete amevunja ukimya na kuagiza
wizara zake mbili kukabiliana na ugonjwa huo kwa dharura.
Ugonjwa huo uliingia nchini tangu mwaka 2010 lakini mlipuko wake
mkubwa ulibainika Machi mwaka huu na hadi jana wagonjwa zaidi ya 400
walikuwa wameambukizwa, huku watatu wakiripotiwa kufariki dunia, akiwamo
Daktari Bingwa wa magonjwa ya akili, Dk Gilbert Buberwa anayezikwa leo,
Dar es Salaam.
Rais jana aliziagiza Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na ile ya
Fedha kushirikiana Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kuchukua hatua za dharura
kupambana nao kwa kuhakikisha vinapatikana vipimo vya kutosha na dawa.
Wachina walazwa
Taarifa kutoka Hospitali ya Aga Khan, Dar es Salaam zilieleza kuwa
wagonjwa waliobainika kuugua homa hiyo hadi jana ni raia hao wa China na
Watanzania wachache wenye historia ya kusafiri nje ya nchi hasa China,
Ufilipino na Kusini mwa India.
Muuguzi katika kitengo cha magonjwa ya kuambukiza cha Aga Khan,
Nyangee Lugoe alisema hospitali hiyo ilianza kupokea wagonjwa tangu
Machi mwaka huu na kuanzia Aprili, raia wengi wa China wamegundulika
kuwa na homa hiyo, ingawa baadhi walitibiwa na kuruhusiwa.
Agizo la Rais Kikwete
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani huko Arusha, Rais Kikwete alisema:
“Hili ni jambo la dharura la kitaifa lazima hatua muafaka zichukuliwe
kudhibiti ugonjwa huu, ambao asili yake ni nchi za Asia na Bara la
Amerika.”
Alisema dalili za ugonjwa huo ambao unasababishwa na mbu aina ya
Aedes Egyptie anayeuma mchana ni homa kali ya kuumwa kichwa, maumivu ya
viungo na kutoka damu puani na kwenye fizi na kupoteza fahamu.
“Napenda kutoa wito mtu yoyote ambaye atapata dalili za ugonjwa
huu, aende mara moja hospitalini ili afanyiwe vipimo badala ya kunywa
dawa,” alisema.
Tayari Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imetangaza kuanza kuchukua
hatua za dharura kukabiliana na ugonjwa huo, ikiwa ni pamoja na
uelimishaji na uhamasishaji wa jamii kuchukua tahadhari.
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Charles Pallangyo alisema jana kuwa
wizara yake imetoa hadhari ya ugonjwa huo kupitia kwa waganga wakuu wa
mikoa na wilaya kote nchini na itatoa mafunzo maalumu kwa watumishi wa
afya ikiwajumuisha madaktari na mafundi maabara ili kuwajengea uwezo
Aidha, wizara hiyo itaanzisha vituo maalumu vya ufuatiliaji wa ugonjwa huo katika hospitali za Mwananyamala, Amana na Temeke.
Ugonjwa kutoka nje
Daktari Kiongozi na Mtaalamu wa Homa ya dengue katika Hospitali ya
Mwananyamala, Dk Mrisho Lupinda alisema upo uwezekano mkubwa kuwa virusi
hivyo viliingia nchini kutokana na mwingiliano na urahisi wa watu
kusafiri kati ya Tanzania na nchi za Mashariki ya Mbali.
“Namna watu wanavyopata nafasi ya kusafiri kwa haraka kwenda
sehemu moja na kurudi kwa shughuli mbalimbali ikiwamo biashara ndivyo
namna maambukizi yanavyoenea kwa urahisi. Hii inawezekana kabisa kwamba
mwingiliano wa kibiashara umechangia kwa kiasi fulani,” alisema.
Alisema ugonjwa huo ni wa kawaida katika maeneo ya kitropiki kwenye
mabara yote, lakini umezoeleka zaidi kwenye nchi za Mashariki ya Mbali
hasa bara la Asia.
Alisema mbu wanaoambukiza ugonjwa huo walikuwapo nchini kwa zaidi ya miaka 300 iliyopita lakini hawakuwa na virusi hivyo.
Hakuna unyanyapaa
Mkurugenzi wa Tiba katika Hospitali ya Aga Khan, Dk Jaffer Dharsee
alisema licha ya ugonjwa huo unaua na kuambukiza, wananchi hawapaswi
kuwa na unyanyapaa kwa waliogua.
“Baada ya taarifa kuenea kwa kasi, kuna watu wameogopa na
wanadhani wale waliopata hawapaswi kuguswa au kusogelewa lakini huu ni
ugonjwa usioambukizwa kwa njia hizo kama ukoma,” alisema.
Alisema mgonjwa wa dengue anahitaji tiba ya dalili zinazojitokeza
na ili asiambukize atahitaji kulala kwenye chandarua hata kama ni
mchana,” alisema.





0 comments:
Post a Comment